SAMATA AJIUNGA RASMI NA TAIFA STARS

Nahodha wa timu ya taifa Taifa Stars,Mbwana Samata amewasili rasmi hapa nchini tayari kwa ajili ya kujiunga na timu ya Taifa kujiandaa na michezo miwili ya kimataifa ya kirafiki iliyo kwenye kalenda ya FIFA.


Baada ya kuwasili katika uwanja wa ndege wa Mwalimu Julias Kamabarage Nyelele jijini Dar es salaam mishale ya saa tisa usiku,Samata amesema kwamba anajiunga na timu ya Taifa kwa lengo moja tu la kupigania taifa lake ili lifanikiwe kufanya vizuri katika mechi hizo mbili.


Alisema kwamba licha ya kuonekana kwake kuwa ni mchezaji wa kimataifa lakini amewataka watanzania kufahamu kuwa Samata ni yule yule wa awali labda kilichobadilika kwa upande wake ni uzoefu katika uchezaji.


Aidha alisema kwamba kwa sasa nguvu zao wanazielekeza kwenye mechi hizo ili wapate ushindi wakiwa nyumbani na amewataka watanzania kutofikilia swala la nafasi iliyopo Tanzania katika ubora wa viwango vya FIFA.


Hata hivyo amedai kuwa licha kuwepo kwa mabadiliko kwenye benchi la ufundi la timu hiyo linaloongozwa na kocha Salum Mayanga, ana imani na kocha huyo kwani si mgeni katika timu hiyo ya Taifa Stars ingawa kutakuwa na mabadiliko ya kiufundishaji kwani kila kocha ana mbinu zake.


Stars inataraji kushuka dimbani siku ya tarehe 25 ya mwezi huu kumenyana na Botswana kisha kucheza mchezo mwingine wa pili na Burundi utakaopigwa tarehe 28 ya mwezi huu,mechi zote mbili zikipigwa kwenye uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.

No comments