AZAM FC KUWAVAA KCCA YA UGANDA

KLABU Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati, Azam FC, kesho Alhamisi inatarajia kukipiga dhidi ya KCCA katika mchezo wa kirafiki utakaofanyika Uwanja wa Phillip Omondi, jijini Kampala, Uganda kuanzia saa 10.00 jioni kwa saa za Afrika Mashariki.
Azam FC ipo kwenye maandalizi makali kwenye kambi yake nchini humo kwa siku 10 ikijiandaa na msimu ujao wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) unaoanza rasmi Agosti 26 mwaka huu.
Kikosi cha Azam FC kiko vizuri kabisa katika kambi hiyo na Kocha Mkuu, Aristica Cioaba na benchi lake zima la ufundi, wamekuwa wakifanya kazi kubwa kukipika vilivyo kikosi hicho pamoja na kuwaunganisha wachezaji kimfumo na kiuchezaji.
Wachezaji wamekuwa wakipokea vizuri mafundisho hayo na kufurahia kiujumla kambi nzima ya hapa Uganda na wamekuwa wakionyesha ushindani mkubwa mazoezini lengo likiwa ni kila mmoja kupata namba kwenye kikosi hicho.
Mabingwa hao wa Ngao ya Jamii na Mapinduzi Cup msimu uliopita wanaodhaminiwa na maji safi ya Uhai Drinking Water na Benki ya NMB, kabla ya mchezo huo wanatarajia kufanya mazoezi jioni ya leo kwenye uwanja huo kwa ajili ya kujiweka sawa.
Mara baada ya mchezo huo, Azam FC inayotarajia kurejea Tanzania Agosti 15, itamalizia ziara kwa mechi nyingine tatu za kirafiki kama ifuatavyo;
11th August: Onduparaka vs Azam FC
13th August: URA vs Azam FC
14th August: Vipers vs Azam FC
Tayari ratiba ya ligi imeshatoka, ambapo Azam FC itafunguwa pazia kwa kucheza ugenini na Ndanda katika mchezo utakaofanyika Uwanja wa Nangwanda Sijaona, Mtwara Agosti 26 mwaka huu.

No comments