WALES KATIKA MTIHANI MZITO WA KUWEKA HISTORIA MBELE YA URENO



Timu ya taifa ya Wales inajiandaa kwa mechi kuu katika historia yake itakapokutana na Ureno mjini Lyon kwa mechi ya nusufainali Euro 2016.
Vijana hao wa Chris Coleman kufikia sasa wamefanya vyema sana katika michuano hiyo ya ubingwa Ulaya na kufika nusufainali mara ya kwanza katika michuano mikuu tangu 1958.
England ilikuwa timu ya mwisho kutoka Uingereza kufika fainali ya Kombe la Dunia au Kombe la Ubingwa Ulaya miaka 50 iliyopita.
"Hatupigiwi upatu kushinda lakini tuna Imani,” anasema meneja Coleman.
Zaidi ya nusu ya raia wote 3 milioni wa Wales wanatarajiwa kutazama mechi hiyo.
Wales watamtegemea sana nyota wao anayechezea klabu ya Real Madrid ya Uhispania, Gareth Bale.
Watakuwa bila Aaron Ramsey wa Arsenal ambaye anatumikia marufuku.


Ureno nao watamtegemea sana Cristiano Ronaldo.
Mara ya mwisho kwa mataifa hayo mawili kukutana ilikuwa Juni mwaka 2000 ambapo Ureno waliondoka na ushindi wa 3-0.

Ureno ndio waliocheza mechi nyingi Zaidi katika historia ya michuano ya ubingwa Ulaya bila kufanikiwa kutwaa ubingwa. Wamecheza mechi 33.
Mechi itakapoanza Ronaldo, atakuwa anasaka bao la kumsaidia kufikia rekodi ya Michel Platini ya kufunga mabao mengi Zaidi katika historia ya michuano hiyo.


No comments