KENYA YASHINDWA KUNYAKUA TAJI KATIKA MCHEZO WA RAGA

Timu ya taifa ya mchezo wa raga ya wachezaji saba kila upande imemaliza ya pili katika michuano ya dunia ya Sevens Series baada ya kufungwa katika mchezo wa fainali na Fiji kwa alama 32-12 jijini Vancouver nchini Canada Jumatatu asubuhi.

Licha ya kutofanikiwa kwa timu hiyo inayofahamika kama Shujaa, wachezaji walionesha mchezo wa hali ya juu katika kipindi chote cha mchuano huo na mashindano hayo.

Fiji ambao ni mabingwa wa michezo ya Olimpiki, wamekuwa wakifanya vizuri dhidi ya Kenya na huu umekuwa ushindi wake wa 34 katika historia ya nchi hizi mbili katika mchezo wa raga.

Ushindi wa Fiji ni kama kulipiza kisasi kwa sababu, mwaka 2016, wakati Kenya iliponyakua taji la Singapore Sevens, iliishinda Fiji alama 30-7 na kurejea na kombe jijini Nairobi.

Kenya sasa inashikilia nafasi ya nane kwa alama 64 katika msururu wa mataifa yanayoshiriki katika michuano hiyo  nyuma ya Uingereza ambayo inashikilia nafasi ya saba kwa alama 70.
Afrika Kusini inaendelea kuongoza kwa alama 109 huku Fiji ikiwa ya pili kwa alama 101.
New Zealand ni ya tatu kwa alama 92.
Mzunguko ujao utafanyika Hong Kong kati ya tarehe 6-8 mwezi Aprili.

No comments