MIEMBENI CITY YATINGA LIGI KUU MSIMU UJAO

Na Sleiman Ussi Zanzibar .
Timu ya Miembeni City wamefanikiwa kutwaa ubingwa wa ligi Daraja la kwanza Taifa Unguja baada ya kuwakandamiza Ngome mabao 2-0 katika mchezo wa mwisho wa 4 bora uliopigwa jana usiku katika Uwanja wa Amaan.
                 
Mabao ya City yamefungwa na Yahya Karoa na Haruna Abdallah “Boban” ambayo yamepeleka furaha klabuni kwao.

Kwa matokeo hayo City imefanikiwa kuongoza 4 bora na kutwaa kombe la daraja la kwanza Taifa Unguja baada ya kufikisha alama 9 kwa michezo mitatu kufuatia mchezo wa awali kuichapa Charawe 2-0, wakaipiga Sebleni United 2-0, na kuwamaliza Ngome 2-0, hivyo City wataungana na Charawe kuinusa ligi kuu msimu ujao.

Mapema Charawe imefanikiwa kuondoka kwenye daraja la kwanza Taifa na kusubiri mfumo gani utumike ili zipatikane timu 12 za msimu ujao wa mwaka 2017-2018, baada ya kupata ushindi wa mabao 3-0 dhidi ya Sebleni United kwenye hatua ya 4 ligi daraja la kwanza Taifa mchezo uliopigwa katika uwanja wa Amaan.

Mabao ya Charawe yamefungwa na Is haka Mzee dakika ya 55, Jumanne Abdallah dakika ya 60 na 71.

Timu 2 za juu kwa daraja la kwanza Taifa kwa kila Kanda (Unguja na Pemba) yani Miembeni City na Charawe kwa Unguja, na zile mbili za Pemba zitaungana na timu 24 zilizobakia kwenye ligi kuu na zitakuwa jumla ya timu 28 kwa Zanzibar nzima, ndipo hapo kwa pamoja watapanga ni mfumo gani utumike ili zipatikane timu 12 za msimu ujao ambapo inasubiriwa imalizike 8 bora ndipo mchakato huo uanze.

No comments