RAIS WA ZANZIBAR ATIMIZA AHADI YAKE KWA WACHEZAJI WA ZANZIBAR HEROES

Na,Sleiman Ussi,Zanzibar
Wachezaji na Viongozi wa Timu ya Taifa ya Soka ya Zanzibar (Zanzibar Heroes) wamekabidhiwa hati zao za viwanja walivyoahidiwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt Ali Mohamed Shein aliyetoa ahadi kwa mashujaa hao Disemba 24, 2017.
Wakikabidhiwa Viwanja hivyo Mashujaa hao huko Tunguu Plan na Waziri wa ardhi, maji, nishati na mazingira Salama Aboud Talib amewataka kuvienzi na kuvitunza kama walivyotakiwa na Dkt Shein.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini Michezo ndio maana ikawazawadia viwanja pamoja na zawadi mbali mbali.
Nae Waziri wa Habari Utalii Utamaduni na Michezo Rashid Ali Juma amesema leo ni siku ya Historia kwa mashujaa hao baada ya kukabidhiwa rasmi Viwanja vyao walivyoahidiwa na Rais wa Zanzibar.
Kwa upande wao wachezaji wa timu hiyo wamefurahishwa kwa kukabidhiwa viwanja hivyo huku wengine wakishindwa kuamini kupata viwanja hivyo kwani hawakutegemea katika Maisha yao kumiliki Kiwanja kikubwa kama hivyo walivyokabidhiwa.
Zanzibar Heroes ilifanikiwa kushika nafasi ya pili katika Mashindano ya Cecafa Senior Chalenj Cup Mwaka jana baada ya kufungwa kwa penalty 3-2 na wenyeji Kenya baada ya kutoka sare ya 2-2 ndani ya dakika 120.

No comments