MCHA ATAMBA KUREJESHA KIWANGO CHAKE

Winga wa kulia wa Klabu Bingwa ya Afrika Mashariki na Kati, Azam FC, Khamis Mcha ‘Vialli’, amesema kuwa kiwango kizuri alichoanza kuonyesha hivi sasa ni mwanzo tu, na kutamba kuwa mashabiki wa timu hiyo wakae mkao wa kupokea mambo makubwa zaidi kutoka kwake msimu huu.
Mcha aliyeteswa na majeruhi ya goti kwa misimu miwili iliyopita kabla ya kurejea dimbani mwishoni mwa msimu uliopita, ameanza kuonyesha cheche zake msimu huu hasa katika mechi nne zilizopita alizoanzishwa kikosi cha kwanza.
Ndani ya mechi hizo nne, Mcha amefanikiwa kufunga jumla ya mabao mawili katika mechi dhidi ya Mbeya City (2-1) na Ruvu Shooting (2-2) na kuchangia pasi tatu za mwisho za mabao katika mechi za Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) zinazoendelea kutimua vumbi.
Mabao aliyotengeneza ni kwenye mechi dhidi ya Mbeya City akimtengenezea kwa krosi bao alilofunga Gonazo Bi Ya Thomas, bao jingine alimsetia Fransisco Zekumbawira wakati Azam FC ilipofungwa mabao 2-1 na Ndanda kabla ya Jumapili iliyopita kufunga bao moja na kupiga kona iliyomaliziwa vema kwa kichwa na kiungo Jean Baptiste Mugiraneza ‘Migi’ dhidi ya Ruvu Shooting.
 Mcha alianza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kufanikisha kurejesha makali yake huku akidai kuwa bila yeye asingeweza kufika hapa.
“Nimegurahishwa sana na kiwango nilichoanza kuonyesha hivi sasa, unajua sikuweza kucheza mechi nyingi msimu uliopita baada ya kusumbuliwa na majeraha ya goti ambayo yalinitesa sana kwa misimu miwili, niluirejea mwishoni na kujaribu kuisaidia timu yangu, namshukuru Mungu kwa sasa nimeanza kurejea vizuri kwenye fomu yangu, nawaahidi mashabiki makubwa zaidi,” alisema.
Alisema anaendelea kufanya mazoezi kwa nguvu ili kujiweka fiti zaidi pamoja na kupokea vema mafunzo bora wanayopewa na makocha wapya kutoka Hispania chini ya Kocha Mkuu Zeben Hernandez na wasaidizi wake.
“Makocha wanafanya kazi kubwa sana, nashukuru tunazidi kuimarika kila kukicha, naamini tutafanya makubwa msimu huu, cha muhimu ni mashabiki kuendelea kuwa pamoja nasi kwa nyakati zote za raha na shida, kwani hii ni timu yao na ipo kwa ajili yao,” alimalizia Mcha.

Itakumbukwa kuwa mbali na Mcha kurejea mwishoni mwa msimu uliopita, alifanikiwa kucheza dakika 691 za mashindano mbalimbali (sawa na mechi saba na dakika 61) ambapo alifunga jumla ya mabao manne na kuchangia pasi mbili za mabao

No comments