CAF MBIONI KUTOA MAAMUZI YA KIJEBA CHA CONGO

Shirikisho la mpira wa miguu barani Africa CAF,wiki hii linataraji kutoa maamuzi juu ya mchezaji wa timu ya vijana ya Jamhuri ya Congo,Langa Lesse Bercy,kufuatia malalamiko yaliyowasilishwa na shirikisho la mpira wa miguu hapa nchini TFF kuwa mchezaji huyo amezidi umri wakati alipokuwa anashiriki michuano ya kuwania kwa fainali za vijana walio chini ya umri wa miaka 17.

Awali mchezaji huyo alishindwa kwenda Cairo kwa ajili ya kufanyiwa vipimo vya kutambua umri wake halisi kwa madai kuwa kipindi hicho alishindwa kuhudhuria kutokana sababu zilizoelezwa kuwa ni machafuko ya kisiasa kwenye sehemu alipokuwa mchezaji huyo.

Aidha kwa mara ya pili zoezi hilo lilishindikana baada mtu husika kushindwa kuhudhuria tena kwenye vipimo hivyo licha ya CAF kuagiza kufanyika kwa jambo hilo.

Endapo CAF itabaini kuwa Congo imefanya udanganyifu kwa kumchezesha mchezaji aliyezidi umri,Tanzania ina matumaini ya kupata nafasi ya kucheza fainali za vijana kwani wao ndio wamepigania jambo hilo hadi dakika za mwisho kwa kufuata taratibu mbalimbali zinazohitajika ikiwemo kukubali kulipa gharama za vipimo.

No comments