YANGA NA URA WATAMBA KUONYESHANA UBABE

Na Said Ally,Zanzibar
Michuano ya Kombe la Mapinduzi mwaka 2017/18 inatarajiwa kuendelea kutimua vumbi hapo kesho katika uwanja wa Amani Visiwani Zanzibar kwa kuzikutanisha Yanga dhidi ya URA ya nchini Uganda huku Mabingwa watetezi wa Kombe hilo Azam FC wakikipiga dhidi ya Singida United.

Kuelekea kwenye mchezo kati ya Yanga na URA,kocha msaidizi wa timu ya Yanga,Shadrack Nsajigwa amesema kwamba kwa upande wao wamejipanga kikamilifu kumenyana na wapinzani wao kutoka nchini Uganda.

Nsajigwa alisema kwamba,URA ni timu nzuri iliyofanikiwa kuzifunga Azam FC na Simba lakini kwa upande wao hawaangalii swala hilo bali kilichopo ni kupambana katika dakika 90 ili wafanikiwe kuingia hatua ya fainali.
Nae kocha msaidizi wa timu ya URA,Kalanzi Hamza kwa upande wake amesema kwamba wanafahamu kuwa Yanga ni nzuri katika michuano ya Mapinduzi inayoendelea kufanyika hapa Zanzibar lakini kikosi chake kipo tayari kwa mtanange huo.

Yanga itamenyana na URA katika nusu fainali ya kwanza hapo kesho mchezo utakaoanza kunako mishale ya saa 10 na nusu jioni wakati nusu fainali ya pili itazikutanisha Azam FC pamoja na Singida United.

No comments